Breaking News

IRAN YAINGIA RASMI VITANI DHIDI YA MAREKANI

Tarehe: 21 Jul, 2026


Rais wa Iran Masoud Pezeshkian amesema nchi yake sasa iko katika kile alichokiita vita kamili dhidi ya Marekani, huku mapigano kati ya pande hizo yakiendelea kushika kasi licha ya juhudi za kidiplomasia za kuyamaliza.

Akizungumza na maafisa wa mahakama mjini  Tehran, Rais Pezeshkian amesema Iran inapaswa kuwa na mtazamo wa uhalisia na kukubali athari za vita hivyo. Ameongeza kuwa uwanja muhimu zaidi wa mapambano kwa sasa ni uchumi na maisha ya wananchi, kulingana na taarifa iliyotolewa na ofisi yake.

Pezeshkian ameonya kuwa endapo shinikizo la kiuchumi litaongeza hali ya kutoridhika kwa wananchi na hali hiyo ikaenea, linaweza kudhoofisha uungwaji mkono wa wananchi kwa serikali. Kauli hiyo inakuja wakati mfumuko wa bei nchini Iran umepanda kwa kasi mwezi Juni kutokana na vita na kufikia karibu asilimia 90 kwa mwaka.

Mwishoni mwa Disemba, maandamano yaliyoanza kutokana na kupanda kwa gharama za maisha yalibadilika na kuwa maandamano makubwa dhidi ya serikali. Mamlaka za Iran zilisema zaidi ya watu 3,000 waliuawa, huku mashirika ya haki za binadamu yaliyo nje ya nchi yakisema idadi ya vifo ilizidi 5,000.

Wakati huohuo, Iran imesema imeyalenga maeneo ya kijeshi ya Marekani nchini Jordan, Kuwait na Syria. Bahrain nayo imesema droni kutoka Iran zililenga mifumo yake ya usafiri wa anga.